Rais William Ruto ameomba msamaha kufuatia mkasa wa mauaji tata ya Shakahola.
Katika mahojiano na vyombo ya habari , Ruto amekiri kwamba kulikuwapo na utepetevu katika mfumo wa kiserikali kuanzia ujasusi, upelelezi, vilevile maafisa wa utawala wakiwamo polisi na machifu.
Ruto amejutia kwamba mhusika mkuu katika kisa hicho Paul Mackenzie alikuwa amefahamika kuwa mtu mwenye mienendo ya kutiliwa shaka baada ya kukamatwa mara kadhaa na kuachiliwa.
Ruto hata hivyo amekana madai kwamba hajachukulia kwa uzito unaofaa baada ya kutozuru eneo hilo kufikia sasa. Badala yake, ameorodhesha hatua ambazo amechukua ikiwmao ya kubuni Tume ya Uchunguzi na Jopokazi la Kutathmini Sheria.
Kadhalika ameeleza kwamba jinsi maafisa wa serikali wamepiga kambi kwenye eneo hilo wakiongozwa na Waziri wa Masuala ya Ndani ya Nchi Prof Kithure Kindiki akikariri kwamba kwa sasa eneo hilo ni eneo la operesheni ya kiusalama na kumsuta kiongozi wa upinzani Raila Odinga kwa kutaka kuingia kwenye eneo hilo.
Kuhusu baadhi ya hatua ambazo huenda zikachukuliwa, Rais amependekeza kwamba viongozi katika sekta ya dini wataruhusiwa kupendekeza namna ya kujisimamia yaani ''Self Regulation'' sawa na ilivyo katika sekta ya habari kupitia Baraza la Vyombo vya Habari.