Njoki Ndung'u aiandikia DCI kufuatia madai ya ufisadi

Jaji wa Mahakama ya Juu, Njoki Ndung'u ameiandikia Idara ya Upelelezi, DCI akiitaka kuanzisha uchunguzi dhidi yake na majaji wengine katika mahakama hiyo kufuatia madai ya ufisadi.

Kwenye barua hiyo, Jaji Ndung'u amesema madai yanayoibuliwa ni yenye uzito na yanapaswa kuchunguzwa ili kubaini ukweli.

Ndung'u ambaye anashikilia kwamba hakusika na sakata hiyo, anazitaka idara za uchunguzi kuharakisha hasa ikizingatiwa tayari Tume ya Huduma za Mahakama, JSC inaendeleza uchunguzi huo.

Aidha anataka DCI kuchunguza iwapo kulikuwapo mawasiliano kati yake na watu ambao wametajwa kwenye sakata hiyo.

Jaji huyo ameshtumiwa kupokea hongo pamoja na wenzake Smokin Wanjala, Mohammed Ibrahim na Jackton Ojwang ili kutoa uamuzi usio wa haki ili kudumisha ushindi wa Gavana wa Wajir, Mohammed Abdi.

Huko Migori,

Gavana wa kaunti hiyo, Okoth Obado amekana madai kwamba alijenga barabara inayoelekea nyumbani kwa Jaji Jackton Ojwang. Obado anasema barabara hiyo ilijengwa kuwafaidi wakazi wala si jaji huyo.

Ikumbukwe mchakato wa kumwondoa ofisini Jaji  Ojwang' ulianza rasmi wikii iliyopita baada ya Tume ya Huduma za Mahakama, JSC kusema kwamba ina ushahidi wa kutosha dhidi yake.

Miongoni mwa madai hayo ni kuwa aliahidiwa kujengewa nyumba nyumbani kwake kwenye Kaunti ya Migori iwapo angeshawishi mkondo wa uamuzi kuhusu kesi kati ya Gavana Obado na kampuni ya Sukari ya Sony.

Related Topics