Waziri Echesa atimuliwa!

Na Mate Tongola,

NAIROBI, KENYA,Rais Uhuru Kenyatta amemtimua Waziri wa Michezo na Utamaduni Richard Echesa.

Wadhifa huo umetwaaliwa na Amina Mohammed ambaye amehamishwa kutoka katika Wizara ya Elimu. Aidha, katika mabadiliko ambayo Prof. George Magoha ambaye amekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Kitaifa la Mitihani ameteuliwa kuwa Waziri wa Elimu.

Aidha, Uhuru amemtimua Katibu Mkuu katika Wizara ya Habari na Mawasiliano Fatuma Hirsi.

Vilevile, Kenyatta ametangaza kuhamishwa kwa Makatibu wafwatao; Susan Mochache ambaye sasa atahudumu katika Wizara ya Afya. Ali Noor Ismail sasa ndiye Katibu katika Wizara ya Vyama vya Ushirika, Dkt. Ibrahim Mohamed atahudumu katika Wizara ya Mazingira na Misitu, Mhandisi Peter Kiplagat Tum Wizara ya Leba, Dkt. Margaret Mwakima Wizara ya Masuala ya Afrika Mashariki, Dkt. Susan Koech Wizara ya Wanyama Pori.

Tangazo hilo limetolewa kupitia agizo la Rais mapema Ijumaa.

Rais Kenyatta amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwapo kwa uwajibikaji na uwazi katika serikali yae ili kumsaidia kutekeleza ajenda zake kuu nne.