Na, Suleiman Yeri
Raila atangaza kuanza kwa ukombozi wa taifa
Saa chache kabla ya kuandaliwa kwa marudio ya uchaguzi hapo kesho muungano wa NASA, umewashauri wafuasi wake kusalia nyumbani wasifike katika vituo vya kupigia kura. Kinara wa muungano huo, Raila Odinga amesema lengo la uamuzi huo ni kuepuka dhuluma za maafisa wa usalama dhidi ya waandamanaji wa muungano huo. Hata hivyo amesema maandamano ya kushinikiza mageuzi yatarejelewa Ijumaa wiki hii, baada ya uchaguzi wa kesho. Aidha ametangaza kuwa jina la National Super Allince, NASA, sasa litabadilishwa.
Katika tangazo ambalo lilisubiriwa kwa hamu na wafuasi wengi wa mrengo NASA, Raila alitangaza hatua tano ambazo muungano huo utachukua ili kuhakikisha kuwa matakwa yao yanatekelezwa na serikali. Hata hivyo kabla ya kuyatimiza amewarai wafuasi wake kususia uchaguzi wa hapo kesho.
Kwanza ametanga kuwa muungano huo utabadili jina kutoka National Super Allince, NASA, sasa litabadilishwa kuwa Vuguvugu la Ukombozi, National Resistance Movement tayari kwa harakati za ukombozi na kukabili dhuluma za serikali ya Jubilee.
Aidha amesema hivi karibuni watawashauri wafuasi wa NASA kususia bidhaa za kampuni ambazo zinafaidika na serikali ya Jubilee vilevile kuanzisha bunge la wananchi ambalo litatafuta mwafaka wa kuimarisha demokrasia nchini.
Vilevile amesema NASA itashinikiza kuandaliwa kwa uchaguzi mwingine wa urais katika kipindi cha siku tisini na ambao utakuwa huru na wa haki.
Wakati uo huo, seneta wa Bungoma Moses Wetangula amerejelea kisa cha kupigwa risasi kwa mlinzi wa Naibu Jaji Mkuu akidai kuwa wanaimani kuwa shambulio hilo lilikuwa limemlenga Naibu Jaji Mkuu.
Aidha kuhusu suala la kutokuwapo kwa majaji watano wa Mahakama ya Juu katika vikao vya kuamua hatima ya kura ya urais, Wetangula amedai kuwa kuna uwezakano majaji hao walitishiwa hivyo kususia vikao hivyo.