Kenya imepiga kengele ya tahadhari kuhusu kuongezeka kwa visa vya usafirishaji haramu wa raia wake kuelekea Asia ya Kusini Mashariki, ikilitaja eneo hilo kama tishio ambako watu wanaotafuta ajira wanadanganywa na kuishia katika mitandao ya ulaghai wa mtandaoni na ajira za kulazimishwa.
Akizungumza na wanahabari jijini Nairobi, Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje, alisema takribani Wakenya 400 wamekumbwa na mtego huo wa mawakala wa uajiri wasio waaminifu wanaotoa ahadi za kazi zenye malipo makubwa nchini Vietnam, Urusi, Cambodia na Myanmar, lakini mwishowe hujikuta katika hali aliyoielezea kama “aina ya utumwa wa kisasa.”