1st November, 2016
Mahakama ya watoto huko Nakuru imepiga hatua na kuwa mahakama ya kwanza barani Afrika kuanzisha mfumo wa dijitali kwenye shughuli zake. Mhisani John Tipper kutoka shirika la Play Kenya Therapy ametoa msaada huo kwa mahakama hiyo ambayo sasa imepokea kamera za video ambazo zitatumiwa na mashahidi hususan walio chini ya umri wa miaka kumi na minane kutoa ushahidi wao kwa njia ya kamera bila kusimama kizimbani mbele ya watuhumiwa. Bwana Tipper alisema kwamba alifikia uamuzi huo baada ya kuona ugumu wanaopitia watoto wanapohitajika kutoa ushahidi mbele ya watuhumiwa waliowafanyia unyama kama vile ubakaji. Hakimu mkazi wa mahakama hiyo Judicaster Nthuku amesifu hatua hiyo, akisema kwamba baadhi ya kesi husambaratika kutokana na woga wa watoto. Hakimu mkuu mkazi wa mahakam hiyo Joe Omido alitoa wito kwa idara nzima ya mahakama kuiga mtindo huo.