Wanafunzi wateuliwa kujiunga na shule za upili
Na Beatrice Maganga
Waziri wa Elimu, Dkt. Fred Matiang'i amezindua rasmi shughuli ya kuyaweka wazi majina ya wanafunzi walioteuliwa kujiunga na kidato cha kwanza katika shule mbalimbali nchini. Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Matiang'i amesema serikali imeweka mikakati ya kuhakikisha madarasa yanaongezwa katika baadhi ya shule ili kuongeza idadi ya wanafunzi wanaosajiliwa. Amesema tayari mpango huo umetengewa fedha katika bajeti ya ziada ili kuufanikisha.
Na huku wanafunzi watakaoteuliwa wakitarajiwa kuanza kujiunga na shule za upili kuanzia Januari tisa, Matiang'i amewaonya walimu wakuu dhidi ya kuwaagiza wanafunzi kununua vifaa vya shule katika maduka fulani. Anasema baadhi ya walimu hao wakuu hushirikiana na wafanyabiashara kuwapunja wazazi kwa kuwauzia bidhaa kwa bei za juu mno ili wapewe asilimia fulani ya faida.
Wanafunzi wote waliopata alama mia nne na zaidi katika Mtihani wa Kitaifa wa Darasa la Nane, KCPE wameteuliwa kujiunga na shule za kitaifa nchini.
Wazazi na wanafunzi wameshauriwa kutembelea tovuti ya www.education.go.ke kupata barua za uteuzi wa wanafunzi hao. Aidha wanaweza kutuma nambari ya usajili kwa nambari 20042.