Mahasibu watakiwa kukabili ufisadi
News
By
Sam Amani
| May 24, 2022
Waziri wa Usalama na Masuala ya Ndani ya Nchi Fred Matiang'i amewataka mahasibu kuwa mstari wa mbele kukabili ufisadi katika sekta ya umma.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kongamano la siku tatu la Mahasibu jijini Mombasa, Matiang'i amedokeza kwamba kesi zote za ufisadi katika taasisi mbalimbali za serikali zimechangiwa na mahasibu ambao wamekuwa wakizindisha kiasi cha fedha zinazohitajika kutekeleza miradi mbalimbali vilevile kutoa huduma kwa umma.
Matiang'i ametoa mfano wa ripoti moja iliyolenga kutathmini matumizi ya fedha katika Idara ya Magereza ambapo matumizi yake yalizidishwa na kufikia takribani shilingi bilioni 6.
Aidha, ameeleza haja ya mahasibu kutunza rasilimali za umma, kuhakikisha zinatumika ipasavyo ili kuepusha hali ya matumizi mabaya ya fedha.
Kongamano hilo linalenga kujadili mbinu za kufufua uchumi hasa kufuatia athari za janga la korona.