Ruto atangaza timu ya watakaowania ubunge Nairobi
News
By
Esther Kirong'
| May 02, 2022
Mwaniaji wa urais wa Chama cha UDA william Ruto ametangaza orodha ya wagombea wa ubunge kwenye Kaunti ya Nairobi.
Katika orodha hiyo, Wakili Nelson Havi atawania Kiti cha Ubunge kwenye eneo la Westlands, John Kiarie atatetea kiti chake cha Dagoretti Kusini kwa tiketi ya UDA, Nixon Korir-Lang'ata huku aliyekuwa mchezaji wa kandanda wa Inter-Milan, McDonald Mariga akiwania ubunge Kibra kwa mara ya pili.
Billian Ojiwa atawania Mathare, Simon Mbugua wa EALA, Starehe, Rabow Hassan Kamukunji, Anthony Waithaka Makadara, George Theuri Embakasi Magharibi, Francis Muriithi akiwania Embakasi Mashariki, Mejja Donk Embakasi ya Kati na David Gakuya, Embakasi Kaskazini huku Ulbunus Kalumba akiwania Embakasi Kusini.
Ikumbukwe Chama cha Azimio la Umoja One Kenya kilitangaza orodha ya wagombea wake wa nyadhifa mbalimbali mwezi uliopita.
Mirengo ya Azimio na Kenya kwanza inayojumuisha UDA, inatarajiwa kuchuana huku kivumbi kikali kikitarajiwa kutifuliwa kwenye uchaguzi mkuu wa Agosti 9.