Wengi wetu hutamaushwa sana na jumbe za aina hii lakini tunalazimika kuishi na ukweli huu mchungu kila uchao. Hivi nikikwambia ya kwamba zipo mbinu za kuepukana na jumbe za aina hii? Ya kwamba kwa hakika unaweza kuzikarabati akaunti hizi ili angalau baada yako kufariki bado utakuwa umezidhibiti kwa njia ambayo hazitaweza kuingililia maisha ya wenzako?
Watu wengi
wanapopanga mazishi yao, hauna budi kupata ya kwamba wao ni wanachama katika
vyama vya mazishi na hata pia huzikarabati vyeti vya kuashiria ni nani
atayemiliki mali yao baada yao kufariki mara kwa mara. Ila ni wachache ambao
huwazia kuhusu akaunti zao za mitandao ya kijamii. Maisha katika karne hii ya
21 yanamlazimu kila adinasi kuwa angalau na simu ya rununu na kompyuta ambazo
hufanikisha akaunti hizi za kijamii ikiwemo Facebook, Twitter, Instagram,
Snapchat, LinkedIn, Pinterest, Tumblr……. … na nyinginezo zaidi.
Wengi wetu hutumia wakati mwingi katika mitandao hii lakini ni kwa nadra sana huwazia kitakachofanyika wanapoenda akhera.
Ni rahisi kufungua akaunti hizi kama hesabu ya 123 ila kibarua cha kuzifunga huwa chenye tashwishi si haba. Hata hivyo, kuwepo kwa tashwishi hizi hakumaanishi ya kwamba hatuwezi kuzifunga akaunti hizi kwani jibu linapatikana katika ufahamu wa muundo wa mitandao hii ya kijamii.
Mtandao wa Facebook ni miongoni mwa mitandao michache ambayo inapeana mfumo wa kupangia kifo. Katika mkataba wao unaofahamika kama Legacy Contract, mtandao huu unampa mwenye akaunti kibali cha kumteua mtu mwingine ambaye atachukua usukani wa akaunti hiyo baada ya mwenye akaunti kufariki. Aliyeteuliwa ana nafasi ya kuwafahamisha marafiki zako katika Facebook kuhusu kufariki kwako. Ana nafasi pia ya kukusanya na kuhifadhi shughuli zako za umma, iwe ni picha, arafa au hata video.
READ MORE
KRA targets 5 million tax filers with WhatsApp option
Content creator focuses antics on mental health
Ila, mtu huyu hana kibali cha kutazama arafa zako kwa hivyo ikiwa ulikuwa na arafa za siri una ukahika wa kuzikwa pamoja nazo. Baada ya hatua hizi, mtandao huu wa Facebook humwezesha mtu huyu kuifunga na kuifuta akaunti hii, kitu ambacho mtandao wa Instagram, unaomilikiwa na kampuni ya Facebook, hauwezeshi.
Hata hivyo, inatakikana mtu anapokarabati vile vyeti vya kuashiria ni nani atakayemiliki mali yao aweze pia kunakili nywila za akaunti zake za mitandao hii ili iwe rahisi kufanikisha huduma hii ya kufunga akaunti hizi.
Ikiwa wewe ni mtumizi wa mtandao wa Google, una kila sababu ya kuridhika kwani mtandao huu unawapa watumizi wake fursa ya kuteua mameneja kumi wa akaunti yake ambao humiliki akaunti yako baada yako kufariki. Ili kufanikisha shughuli hii, mtumizi wa akaunti katika Google anatakiwa kuenda katika kitengo cha Help and Support katika akaunti yake. Katika kitengo hiki kuna kijisehemu kinachofahamika kama Inactive Account Manager ambacho kinampa mwenye akaunti mwongozo wa kuwateua mameneja hawa.
Mitandao
ya Twitter na LinkedIn pia inampa fursa mmoja wa jamaa ya marehemu kufunga na
kuzifuta akaunti za mwendazake. Hata hivyo, katika harakati za kufanikisha
shughuli hii, jamaa huyu anatakikana kutoa cheti cha kifo cha marehemu.
Katika mtandao wa WhatsApp, ni rahisi zaidi kufunga akaunti huko kwani ni vitu viwili tu vinavyotakikana- kodi ya nchi na nambari ya simu. Hivyo basi, inakuwa rahisi kufuta jumbe zozote zilizoko katika akaunti hii na pia zilizohifadhiwa bila mtafaruku wowote.