Kuhukumu ni kufanya lile jambo linaloitwa judgement. Ni ile hali ya kutoa uamuzi kuhusu jambo fulani linalohusu watu wengine. Vile vile, unaweza kuwa kati ya waathiriwa na ujipate ukihukumu mwenzio.

Kwa hivyo, hili ni jambo la kawaida maishani mwetu kwa sababu kila mtu huwa na mtazamo tofauti na mwenziwe kuhusu swala fulani.

Kuna mengi ambayo hutokea maishani mwa mtu. Mengine ambayo hukera hata kabla ya kuwaza. Haya ni ya yale mambo ukiona au ukiskia unakereka tu bila kutaka kujua sababu ya jambo lenyewe.

Katika maisha yetu ya kila siku huwa tunajipata katika hali hii sana sana. Tunajipata katika hali ya kuhukumu wengine, si kwa kupenda kwetu, ila ni kwa kuwa fikra zetu zinawaza kuwa jambo fulani si njema.

Utamwona mtoto anaendesha baiskeli barabarani na ukaishia kukasirika na kushangaa mzazi wake yu wapi hadi kufikia kiwango cha kumwacha mtoto atoke nje, bila kujua kwamba labda mtoto ametoweka nyumbani na kwenda nje bila ruhusa ya mzazi wake. Hii ni mojawapo tu ya mambo ambayo watu hujipata wakihukumu wengine bila kuwaza upande wa pili.

Katika maisha yaya haya ambayo wengi hujipata wakihukumu wenzao utapata wengine wameifanya kuwa ndio kazi kuu kwao.

Waamkapo, walalapo na hata waotapo wao wanahukumu tu wenzao. Yaani hawana lingine wanalowaza hata kidogo kando na kuchungulia majirani.

Watu wenye tabia hii ya kuhukumu hukumu huwa hawapendi kuona mtu akipiga hatua maishani.

Hawa hukaa nje kuwaza mbona jirani yule alinunua gari? Mbona amejenga nyumba kubwa? Mbona watoto wake wamebadilisha shule na kwenda za kifahari? Yaani hukumu tu za kiwivu huwajaa mioyoni. Huwa hawana furaha kwa mafaniko ya wengine.

Gere hii huwa imewachoma hadi kuwafanya kuishia na majibu kama vile, alijiunga na kikundi cha waabudu mizimwi, yeye hutoa watu kafara na aliiba mali ya umma kufika aliko. Huku tukitafakari kuhusu hawa vyema kuweka bayana kwamba hakuna aliye mkamilifu.

Hakuna asiye na dosari ila kosa la mtu lisifanye uishie kumhukumu vibaya. Jaribu kutazama wema wake pia, na kujua kwamba kuna mengi mazuri anayofanya.

Tabia ya watu kuhukumu wenzao ni tabia mbaya isiyopendeza. Tunapokuwa katika uso wa dunia usiokuwa na huruma na mara kwa mara hutungurumia sote, kuwa mwema kwa wenzio.

Hakikisha kwamba jirani, swahiba na jamaa wanakuona mtu wakutegemewa na si mtu wa kutengwa kutokana na hulka yako ya kuhukumu wenzako kwa kujiona bora.

Wewe pia hufanya makosa na wengine hukuhukumu, ila hawajui unayopitia na yaliyokusibu hadi ukatenda jambo fulani. Aisee, tuwe wema. Hata mui huwa mwema.