Huenda shughuli za usafiri zikatatizika kote nchini kuanzia Jumatatu wiki ijayo baada ya Muungano wa Wahudumu wa magari ya uchukuzi wa umma kuwashauri wanachama wao kushiriki mgomo. Muungano huo umeitisha mgomo huo kulalamikia kuanza kutekelezwa kwa sheria za trafiki maarufu sheria za Michuki.

Ikumbukwe wahudumu wote wa magari walipewa hadi tarehe kumi na mbili mwezi huu yaani Jumatatu kuhakikisha kuwa wanazingatia sheria hizo kama vile, kuweka vidhibiti mwendo na mikanda ya usalama katika magari yao, la si hivyo adhabu kali zitachukuliwa.

Hapo jana Waziri wa masuala ya Ndani ya Nchi Fred Matiangi, aliongoza uzinduzi wa oparesheni kali itakayoanza Jumatatu. Matiangi alisema hatua hiyo inalenga kupunguza visa vya ajali za barabarani.

Takwimu za hivi punde za Mamlaka ya Usalama Barabani NTSA zinaonesha kwamba watu elfu mbili mia sita ishirini na sita wameaga dunia na wengine elfu tatu mia mbili na arubaini wamejeruhiwa kufuatia ajali za barabarani mwaka huu pekee.