Seneta wa Nairobi, Johnson Sakaja amewashutumu vikali maseneta wenza waliomwakilisha mahakamani Gavana Mike Sonko, anayekabiliwa na tuhuma za ufisadi.

Akihojiwa na redio moja nchini mapema leo, Sakaja amesema Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Seneti Kipchumba Murkomen na Seneta wa Makueni Mutula Junior, walikiuka sheria za Seneti ikizingatiwa wajibu wao ni kulinda rasilimali na utendakazi wa kaunti, si kuwatetea washukiwa wa ufisadi. Sakaja amesema suala wawili hao kumtetea Sonko mahakamani, imewaonesha wawili hao kuunga mkono ufisadi.

Sawa na Wakenya wengi waliokosoa hatua ya wawili hao kuwa miongoni mwa mawakili wa Sonko, Sakaja amesema wawili hao walifaa kuwapa majukumu ya utetezi mawakili wengine katika kampuni zao za uwakili badala ya kujiwasilisha mahakamani.

Ikumbukwe suala hilo limezua mjadala mkali miongoni mwa Wakenya, huku baadhi wakisema hapakuwapo na kosa kwa wawili hao kumtetea Sonko kwani hawakufika mahakamani kwa majukumu ya useneta.