Siku moja tu baada ya Kundi la Wabunge Wanawake la Embrace kuzuru Kaunti ya Kisumu huku likitumia magari yaliochapishwa picha za Rais Uhuru Kenyatta na Kinara wa ODM Raila Odinga, Mbunge wa Malindi Aisha Jumwa amelisuta kundi hilo akisema linaendesha kampeni za mapema. Kwa mujibu wa Jumwa, kundi hilo linatumika kuendeleza siasa za chuki zilizopitwa na wakati.
Akizungumza katika Wadi ya Kaloleni Kaunti ya Kilifi wakati wa ufunguzi wa jengo moja katika Shule ya Msingi ya Gogoraruhe, Jumwa amesema kwa sasa Wakenya wanahitaji maendeleo wala si siasa za kupakana tope.
Amesema Rais Kenyatta alionya kwamba siasa zinapaswa kusitishwa ilhali kundi la Embrace linapiga siasa za mwaka wa 2022 bila kujali kauli ya Rais anayetaka kuwahudumia Wakenya.
Jumwa amemsihi Rais kulikomesha kundi hilo dhidi ya kuzichapisha picha zake kwenye magari yao hasa ikizingatiwa huu si wakati wa siasa.
Wakati uo huo, Jumwa amesema Kundi la Wabunge Wanawake la Inua Mama litaendeleza shughuli zake mashinani ili kuwapiga akina mama jeki kibiashara lengo likiwa kuinua uchumi mashinani.
Jumwa ameandamana na Mbunge wa Kalolelni Paul Katana, Seneta Mteule Chrsitine Gona na wawakilishi wadi kadhaa wa Kilifi.