Na Geoffrey Mung’ou
Washikadau mbalimbali wanaendelea kupaaza sauti kuhusu umuhimu wa kuandaliwa kwa uchaguzi huru na wa haki. Jumanne Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Nchini lilikutana na wahariri wa vyombo vya habari nchini na kutaja mambo sita ambayo yanaweza kuhujumu lengo la kuandaliwa kwa uchaguzi ulio huru iwapo hayatadhibitiwa mapema.
Katika kampeni chini ya kaulimbiu, Uchaguzi wa Amani, wa Kuaminika na Viongozi Waadilifu, Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki limesisitiza haja ya sajili ya wapigakura kufanyiwa ukaguzi wa kuondoa dosari ili kuepusha mivutano ya kisiasa.
Askofu Cyprian Nyamwamu, ambaye ni Afisa wa Uongozi na sera katika baraza hilo amesema Masuala mengine ambayo yanaweza kutatiza uhuru wa uchaguzi ni mivutano kuhusu uteuzi wa vyama na suala la wanasiasa kutilia shaka uadilifu wa makamishna wa Tume ya Uchaguzi. Aidha limetaja hatua ya Mahakama Kuu kufutilia mbali tenda ya shilingi biloni 2.5 ya uchapishaji wa karatasi za kura kuwa kimojawapo cha vizingiti vya maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao. Askofu Nyamwamu tena.
Naye Mwenyekiti wa baraza la hilo, Alfred Rotich amewashauri Wakenya kutokubali kuhongwa na wanasaisa, huku akiwashauri kupiga kura baada ya kutathmini vyema sera na rekodi zao za maendeleo.
Linus Kaikai aliyekiwakilishi Chama cha Wahariri Nchini katika kikao hicho amewashauriwa kuiga mfano wa viongozi wa awali wa dini kama vile Moris Otunga, Manases Kuria, Ndingi Mwana Nzeki, Alexander Muge, John Njue miongoni mwa wengine, waliopigania kwa dhata demokrasia na haki za Wakenya. Mbali na kuandaa vikao mbalimbali kuanzia sasa hadi uchaguzi utakapoandaliwa Agosti 8, baraza hilo la Maaskofu wa Kanisa Katoliki, limeahidi kushirikiana na Tume ya Uchaguzi, IEBC na washikadau wengine ili kufanikisha uchaguzi huru na wa amani.