Na Mate Tongola
NAIROBI, KENYA, WATU sita wameuliwa na wanamgambo wa Al Shabaab kuyavamia mabasi mbili eneo la Elwak, Kaunti ya Mandera.
Shambulizi hilo limetekelezwa kati ya miji ya Wargadud na Elwak baada ya wanamgambo hao kuyamininia risasi magari hayo katika kituo cha Corner S mwendo wa saa nne asubuhi.
Kamanda wa eneo la kaskazini mashariki Mohamed Saleh amesema kuwa watu sita akiwemo polisi wa akiba waliuliwa kwenye shambulizi hilo huku wengine wakiwachwa na majeraha.
Inaarifiwa kuwa mabasi hayo yalikuwa chini ya ulinzi wa polisi yaliposhambuliwa.
Ni jana ambapo Kaimu Naibu wa Kamishna wa Mandera Mashariki Yonah Nyawir alitangaza kupigwa marufuku kwa usafiri wa wageni wanaoingia au kuondoka kaunti hiyo kwa basi hadi mfungo wa Ramadhan uishe.
Kwa mujibu wa kamati ya Usalama ya Kaunti hiyo, wasafiri wanaotumia basi mara nyingi hushambuliwa na makundi ya kigaidi.