Jinsi Sonko alivyo toroka jela akiwa amevaa buibui

Gavana Mike Sonko.

Ama kwa hakika waliosema kuwa “pesa zilivunja mlima”, kweli hawakuwa na mzaha wa maana hiyo. Na tamaa nayo, pia wahenga walisema ilimpasua “fisi” msamba!

Mfanyabiashara anayedai kuwa mlalamishi wa kesi iliyomtorosha Gavana wa Nairobi Mike Sonko Mbuvi kutoka jela ya Shimo la Tewa mnamo mwaka 1998, amerejea tena mahakama kuu ya Mombasa kuwasilisha kesi mpya kudai alipwe zaidi ya shilingi milioni 10 anazodai kulaghaiwa miaka 21 iliyopita.

Kwa kuwa gavana Sonko ni “moto wa kuotea mbali”, mfanyabiashara huyu mwenye asilia ya kihindi amekuwa amekunja mkia wake muda wote huu hadi punde ripoti ilipojitokeza juzi kwamba Gereza la Shimo la Tewa lapendekeza mfungwa wao arejeshwe jela kukamilisha kifungo chake.

Hata hivyo, mfanyibiashara huyo hajakata tamaa kwani anategemea mkono wa sheria kuchukua mkondo wake baada ya kuwasilisha kesi mpya katika mahakama kuu ya Mombasa akitaka Sonko amlipe zaidi ya shilingi milioni 10 anayodai kulagaiwa kutoka kwake na Gavana wa Nairobi.

Ni jamaa huyu huyu ambaye wakati mmoja alimpiga teke na kumshika mashati gavana siku za nyuma alipomkuta ameshikwa na polisi katika kituo cha Central, Mombasa.

“Nilikuwa na hasira mno na wala sikujitambua. Niliona tu nimemrushia teke Sonko niliposikia amebanwa kidogo katika kituo cha Central, Mombasa,” anakiliwa mfanya biashara huyu alipoonekana mapema wiki hii akiwasilisha upya kesi yake ya kudai tena gavana katika mahakama kuu ya Mombasa.

Ripoti kwamba gavana wa kaunti ya Nairobi Mike Mbuvi Sonko kuwa bado hajamaliza kifungo chake cha miezi 12 katika gereza la Shimo la Tewa, Mombasa, zimezua mchipuko mpya zaidi.

Mfanya biashara anayedai kuwa mlalamishi wa kesi yake amejitokeza upya na duku duku za upelelezi wa ndani jinsi alivyotoroka jela zikijitokeza zaidi.

Kulingana na habari za ndani kutoka kwa baadhi ya maafi sa wa magereza ambao hawakutaka majina yao yatajwe, waliokuwepo wakati wa kisa hicho cha mwaka 1998, wanasema kwamba njama ya Gavana Mike Sonko kufaulu kutoroka jela huenda ikawa ilichangiwa na hongo na usaidizi wa wasimamizi wa magereza ya Shimo la Tewa nyakati hizo ambao wamestaafu sasa.

Kupanga njama Upelelezi unazindua kuwa wakati Sonko alipohukumiwa kifungo chake, yaaminika kamwe haikumchukua hata siku mbili kubuni njama ya kukwepa kororokoro za magereza ya Shimo la Tewa. Kwanza, inaelezwa na wasimulizi walioshuhudia kisa hicho kwamba alitumia uwezo wa hela zake kupanga njama ya kuwa mgonjwa ili aweze kulazwa katika hospitali ya magereza ya Shimo la Tewa.

“Gavana huyu mjanja alilazwa katika kituo cha afya cha hapa gerezani lakini kufi kia asubuhi ikasemekana kwam-ba amezidiwa na ugonjwa hivyo apelekwe kwa matibabu zaidi katika hospitali kuu ya Mkoa ya Makadara (Coast General Hospital),” atoboa afi sa mmoja ambaye amestaafu lakini alikuwepo wakati huo wa kisanga mbinu.

Akiwa katika hospitali kuu ya mkoa mjini Mombasa, Sonko twaambiwa ndio aliweza kucheza karata zaidi kwanza kwa kuwafurahisha askari wa magereza waliopewa zamu ya kumlinda kitandani.

Baadhi ya askari wa magereza wa Shimo la Tewa, wanakumbuka kwamba wakati huo kila mmoja wao alitamani kupewa zamu ya kumpiga doria mfungwa Mike Sonko kwani waliweza kurarua viazi vya “chips” kwa kuku na pia marupurupu ya shilingi mia tano kwa siku.

“Alikaa kati ya siku mbili au tatu hospitalini lakini baadaye tukaarifi wa na usimamizi wa magereza hapa kuwa kuna mfungwa ametorokea hospitalini Mombasa,” azungumza askari mmoja aliyetaka jina lake libanwe.

Vazi la buibui Wanaokumbuka vyema kisa hiki, wanazungumzia mpango baina ya usimamizi wa magereza wakati huo na askari waliokuwa wako zamu ya kushika doria hospitali kumlinda Gavana Sonko walioagizwa kulegeza pingu na kuvaa miwani ya mbao ili mfungwa aponyoke.

Na kweli, yaaminika mpango huo ulifanikishwa na wageni walioruhusiwa kumtembelea Sonko hospitalini wakiwa wamebeba vazi la “buibui” ili wakati wa kutoroka wengi wasimtambue.

Swali, lilikuwa ni vipi mtu amletee buibui hadi kitandani ilhali askari wa magereza wanatakiwa kumweka pingu mfungwa akishikanishwa na kitanda chake? Kulingana na habari zaidi za ndani, yasikitisha kwamba askari wawili wa magereza ambao siku hiyo walikuwa zamu ya kumlinda Sonko, walipoteza kazi yao kwa kufutwa.

Msimamizi wa gereza la Shimo la Tewa wakati huo, afi - sa Daniel Mutua Ndambuki kamwe hakuguswa hadi kustaafu kwake hivi majuzi. Mfanyibiashara mmoja mashuhuri wa Mombasa wiki hii amejitokeza na kusema kuwa yeye ndiye aliyechangia kukamatwa na kufungwa jela kwa Gavana wa Nairobi mnamo mwaka 1998.

Mfanyibiashara huyo mwenye asili ya kihindi amedai kwamba Gavana Sonko alimhadaa mamilioni ya pesa, jambo lililomlazimu kupiga ripoti akamatwe na kufunguliwa mashtaka katika mahakama ya Mombasa.

Tajiri huyu ambaye jina lake pia tumelibana kwa sababu ya usalama wake, amesema kwamba alishangazwa na habari kwamba Mike Mbuvi Sonko alikosa kumaliza kifungo chake katika gereza la Shimo la Tewa. Hata hivyo, inasemekana kwamba katika dukuduku za kufanya upelelezi wake wakati huo (1998), alipata kufahamishwa kwamba Mike Mbuvi ‘Sonko’ alitoroshwa jela na baadhi ya askari wa jela wa gereza la Shimo la Tewa.

Anadai kwamba askari waliohusika walimfanya na kusikizana na Sonko ajidai kwamba ni mgonjwa ili apate kupelekwa hospitalini. Mfanya biashara huyu hali kadhalika anasimulia taarifa sawa na ile tuliyoipata kutoka kwa baadhi ya maaskari jela ndani ya gereza la Shimo la Tewa.

Yeye pia anasimulia kwamba njama zao yadaiwa kutimia pale walipokubaliwa kumpeleka Sonko katika hospitali kuu kuu ya Mkoa wa Pwani ya Coast General. Ni hapa ambapo kulingana na mlalamishi kwamba ndipo walipanga njama ya mwisho ya kumtorosha akiwa amevalia “buibui”.

Hata hivyo, mfanyibiashara huyo hajakata tamaa kwani aliwasilisha kesi mpya katika mahakama kuu ya Mombasa akitaka Sonko amlipe zaidi ya shilingi milioni 10 anayodai kumlagaiwa kutoka kwake na Sonko.

Kwa wakati mmoja, mfanyibiashara huyu anadai kupandwa na hasira jambo lilimpelekea kumpiga Sonko teke kadhaa katika kituo cha polisi cha Central, Mombasa baada ya kupata kwamba alikuwa amekamatwa na kupelekwa hapo.

Katika taarifa za magereza zilizowasilishwa kwa tume ya kupambana na ufi sadi nchini ya EACC, kuambatana na vyombo vya habari, vinamlenga gavana Sonko kwamba mnamo mwaka 1998, mwezi Machi tarehe 12 alikabiliwa na shtaka la kukweka mahakama hivyo akaamuriwa kulipa faini ya laki mbili (200,000) lau afungwe kifungo cha miezi sita. Ripoti zaonyesha hakulipa na akasukumwa ndani katika gereza la Shimo la Tewa.

Mnamo siku hiyo hiyo, Sonko pia alihukumiwa na mahakama katika kosa lingine, kulipa shilingi laki tano (500,000) ama abanwe jela kifungo kingine cha miezi sita. Kesi yake ya kwanza ilikuwa nambari CF 675/97 ilhali hii ya pili inatajwa kuwa nambari CF 1727/96.

Hii ina maana alikuwa ahudumie kifungo cha mwaka mmoja (miezi 12) gerezani. Alligizwa gereza la Shimo la Tewa na kukabidhiwa nambari P/No SHO/477/1998 yake ya mfungwa ambapo alitarajiwa kukamilisha kifungo chake kufi kia tarehe 11 mwezi Machi mwaka 1999 lakini yalishangaza wengi kwani kufi kia tarehe 16 mwezi Aprili, 1998, mfungwa Mike Gideon Mbuvi ‘Sonko’ alikuwa ametoweka jela mfano wa msanii wa Afro-Sinema!

Mbiu ya mgambo Taarifa hii ya EACC inaendelea kutujuvya tena kuwa miaka miwili baadaye, mnamo Novemba 15, mwaka wa 2000, msimamizi mkuu wa magereza katika gereza la Industrial Area, Nairobi alimpigia mbiu ya mgambo msimamizi mwenzake wa gereza la Shimo la Tewa wakati huo kumwaarifu kuwa yule mfungwa wake aliyetoroka awali jela sasa amekamatwa asubiri kushindiliwa mashtaka zaidi hivyo awahi.

Yote hayo yakawa ni mjango tu! Kufi kia hapo, Gavana Sonko alikuwa amewekwa kwenye orodha ya fungu la wafungwa sugu kulingana na usimamizi wa idara ya magereza nchini hivyo kuilazimu kumsukuma kwa gereza la masugu zaidi la Kamiti Maximum Prison mnamo mwezi Februari ya tarehe 12, mwaka 2001. Hapa, alipewa nambari nyingine ya mfungwa, KAM/1255/001.