Seneta McCain afariki dunia

Seneta wa Marekani mwanachama wa Republican John McCain, ambaye alikuwa mgombea wa chama hicho katika uchaguzi wa  urais mwaka wa 2008, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 81. Kifo chake kimejiri ikiwa ni miezi 13 baada ya kufichua kuwa anaugua saratani ya ubongo.

Aliamua siku ya Ijumaa kusitisha matibabu ya ugonjwa huo ambao uligundulika Julai 2017. Alikuwa mkosoaji mkubwa wa Rais Donald Trump na ni mwezi uliopita tu ambapo alimkosoa vikali kwa kushindwa kumkabili Rais wa Urusi Vladmir Putin.

MaCain ambaye alikuwa rubani wa jeshi la wanamaji, alishikiliwa kama mfungwa wa vita nchini Vietnam kwa zaidi ya miaka mitano, wakati ndege yake ilipodunguliwa kaskazini mwa Vietnam mwaka wa 1967.

Aliingia bunge la Marekani mwaka wa 1983 kutokea Arizona na akahudumu katika baraza la Seneti tangu mwaka wa 1987. Rais Trump na Aliyekuwa Rais Barack Obama ni miongoni mwa viongozi waliotuma risala za rambirambi kufuatia kifo cha McCain.