PODCASTS

Habari

  • Mazingira

    Uhai wa Ziwa Victoria

    Wakazi wa kaunti ya Kisumu wametakiwa kuwashinikiza viongozi wapya waliochaguliwa eneo hilo kushughulikia kwa haraka kusafishwa kwa ziwa Victoria ambalo ni kitega uchumi kwa asili mia kubwa ya wakazi wa eneo hilo. Akitoa wito huu, Jeppe Kolding ambaye ni mhadhiri katika chuo kikuu cha Bergen nchini Norway, amesema kuwa kwa ushirikiano na wenyeji, serikali ina uwezo wa kulisafisha ziwa hilo na hivyo kukabiliana na umasikini ambao unawaadama wenyeji. Mhadhiri huyo ambaye amefanya utafiti kuhusu ziwa Victori kuanzia mwaka 2005, anasema sharti baraza la jiji la Kisumu lishughulikie kwa haraka suala la maji taka ambayo huelekezwa katika ziwa hilo na hivyo kuhatarisha viumbe vya majini wakiwemo samaki. Katika mahojiano ya kipekee na Radio Maisha mjini Kisumu baada ya kongamano la siku mbili lililowaleta pamoja wataalam wa masuala ya uvuvi chini ya mwamvuli wa Kituo cha Kimataifa kinachoshughulikia masuala ya mazingira, ELCI.

    0 Responses

    Posted on April 19, 2013 na Mate Tongola

  • Usalama

    9 Wauawa Mjini Garissa

    Idadi ya watu walioaga dunia kwenye shambulizi alhamisi usiku mjini Garissa imefikia 9, baada ya wengine watatu kufariki wakikimbizwa hospitalini. Hii ni baada ya watu wasiojulikana kuvamia hoteli moja mjini humo wakiwa wamejihami kwa bunduki aina ya AK-47 na kuwamiminia risasi wateja waliokuwa ndani ya hoteli hiyo kwa jina 'Kwa Chege'. Mkuu wa polisi mkoa wa kaskazini mashariki Charlton Muriithi ameiambia Radio Maisha kuwa kufikia sasa hawajabaini lengo la mauaji hayo ambayo yamesababisha taharuki kutanda mjini Garissa. Ikumbukwe kuwa mapema mwezi huu mwanafunzi aliuawa huku watu wengine watatu wakijeruhiwa baada ya watu waliojihami kutekeleza uvamizi katika kioski kimoja mjini humo. Vile vile, mwanzoni mwa mwezi Aprili, maafisa wawili wa polisi waliuawa na watu wanaoaminika kuwa wafuasi wa Al Shabaab.

    0 Responses

    Posted on April 19, 2013 na Mate Tongola

  • Mishara

    Wabunge Watishia Kuibandua SRC

    Wabunge wametishia kuibandua Tume ya Kuratibu Mishahara ya watumishi wa umma kutokana na hatua yake ya kupunguza mishahara yao. Tayari mbunge wa Igembe Kusini Mithika Linturi ametangaza kuwasilisha ombi kwa spika wa bunge la taifa, kutoa nafasi kwa hoja ya kuitaka tume hiyo ivunjwe huku akidai kuwa Tume imekwenda kinyume na katiba. Hata hivyo, Wakili Bobby Mukangi ambaye alihusika katika kuandika katiba anasema kwamba bunge halina Mamlaka anayodai Linthuri. Anasema tume ya kuratibu mishara ya watumishi wa umma ni huru na haiwezi kushinikizwa na yeyote inapotekeleza majukumu yake. Kwa mujibu wa Katiba tume hiyo ndiyo yenya mamlaka ya kuratibu mishahara ya watumishi wa umma wakiwemo wabunge.

    0 Responses

    Posted on April 19, 2013 na Callen Omae

  • Msiba

    Bi Kidude Afariki

    Mwanamuziki mashuhuri wa nyimbo za taarabu kutoka Zanzibar Bi. Kidude, ameaga dunia. Bi. Kidude kwa jina halisi Fatuma Binti Baraka amefariki jumatano asubuhi akiwa na zaidi ya miaka 100. Anafahamika sana kutokana na nyimbo zake kama vile Muhogo wa Jang’ombe na Yalaiti. Alianza kuimba mwaka 1920 na amewakuza wanamuzika mbalimbali nje na ndani ya ukanda huu wa Afrika Mashariki. Vilevile amekuwa akitoa mafunzo ya unyagoni kwa mabinti wa Zanzibar. Inadaiwa kuwa amefariki kutokana na maradhi yanayohusishwa na umri mkongwe.

    0 Responses

    Posted on April 17, 2013 na Geoffrey Mung'ou

  • Usalama

    Wananchi kuhakikishiwa Usalama

    Rais Uhuru Kenyatta ameitaka idara ya polisi kuhakikisha kuwa usalama unaimarishwa kote nchini. Akizungumza alipokutana na wanatume ya huduma za polisi, Uhuru amesema kuwa ni haki ya kila mwananchi kuishi katika mazingira salama na kuongezea serikali yake itashirikiana kikamilifu na tume hiyo ya huduma za polisi katika juhudi za kuibadilisha idara ya polisi. Wakizungumza katika mkutano huo, mwenyekiti wa tume hiyo Johnston Kavuludi na inspekta mkuu wa polisi David Kimaiyo wamemhakikishia Rais Uhuru kujitolea kwao katika kuwahakikishia wakenya usalama. Aidha, wawili hao wamemwarifu Uhuru kuhusu hali ya usalama nchini pamoja na changamoto zinazokumba idara zao. Viongozi wengine waliohudhuria mkutano huo ni mwanasheria mkuu wa serikali Prof. Githu Muigai, mkuu wa utumishi wa umma Francis Kimemia na mwenyekiti wa tume ya huduma za umma Prof. Margaret Kobia.

    0 Responses

    Posted on April 17, 2013 na Mate Tongola

  • Mchezo wa Kuigiza

    'Shackles of Doom' Kuendelea

    Mahakama Kuu ya Nairobi, yameondolea mbali agizo lililokuwa limetolewa kuizuia Shule ya Upili ya Wasichana ya Butere kuendeleza mchezo wake wa kuigiza kwenye tamasha za taifa mjini Mombasa. Jaji wa mahakama hayo David Majanja ametoa uamuzi huo kutokana na kesi iliyokuwa imewasilishwa mahakamani humo na mwanaharakati Okiya Omtatah kupinga marufuku iliyokuwa imetolewa kuzuia mchezo huo. Agizo hili linamaanisha kuwa shule hiyo sasa ina kibali cha kushiriki mashindano ya taifa ya tamasha za muziki mjini Mombasa. Mchezo huo unaitwa Shackles of Doom. Wizara ya Elimu ilikuwa imeamuru Kamati ya Taifa ya Maandalizi ya tamasha za muziki kupiga marufuku shule hiyo kuendeleza mchezo huo kwa madai kwamba unaeneza chuki. Hali hiyo ilichochea hisia kali miongoni mwa wasimamizi wa shule hiyo, baadhi ya viongozi na wazazi magharibi ya nchi na hata wanaharakati.

    0 Responses

    Posted on April 17, 2013 na Geoffery Mung'ou

  • Kesi ICC

    Ruto Aomba kutojiwasilisha

    Naibu Rais William Ruto amewasilisha waraka katika Mahakama ya Mataifa Kuhusu Uhalifu ICC, kutaka kupewa kibali cha kutohudhuria kesi dhidi yake na badala yake kuwakilishwa mahakamani humo na mawakili wake, huku akifuatilia kesi hiyo kwa njia ya video. Aidha Ruto kupitia wakili wake Karim Khan amesema atafika mahakamani humo wakati wa kuanza kwa kesi hiyo, na wakati wa kutolewa kwa uamuzi. Amesema hali hiyo itamwezesha mteja wake kushughulikia masuala ya uongozi wa taifa, wakati ambapo kesi hiyo itakuwa ikiendelea. Ikumbukwe kuwa kesi dhidi ya Ruto na mwanahabari Joshua Arap Sang itaanza tarehe 28 mwezi ujao, huku kesi dhidi ya Rais Uhuru Kenyatta ikianza tarehe 9 Julai mwaka huu.

    0 Responses

    Posted on April 17, 2013 na Geoffrey Mung'ou

  • Vifaa vya Uchaguzi

    Mkurugenzi wa Mashtaka AAGIZA

    Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma Keriako Tobiko ameteua kamati itakachoshirikiana na Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi EACC, katika uchunguzi dhidi ya ununuzi wa mitambo ya BVR na kilichofanya ishindwe kuhudumu katika vituo vingi wakati wa upigaji kura. Kikosi hicho kitaongozwa naye Kioko Kamula na kitashirikiana na EACC katika uchunguzi huo uliopendekezwa na majaji wa Mahakama ya Juu kwamba baadhi ya taratibu za Tume ya IEBC zifanyiwe uchunguzi wa kina. Katika maamuzi yao, majaji hao 6 walisema ilionekana kwamba uchaguzi mkuu ulikumbwa na hitilafu kadhaa, lakini mlalamishi mkuu Raila Odinga hakutoa ushahidi wa kutosha kuthibitisha kwamba uchaguzi huo ulikumbwa na udanganyifu. Kwa maana hiyo walitupilia mbali rufaa yake ya kupinga ushindi wa Uhuru Kenyatta. Maamuzi hayo yametolewa jana kwenye kikao cha majaji hao ambacho hakikuzidi dakika tatu.

    0 Responses

    Posted on April 17, 2013 na Mate Tongola

  • Usalama

    Wafungwa Wawili wauawa, Siaya

    Wafungwa wawili Wilayani Siaya wameuawa kwa kupigwa risasi na maafisa wa polisi walipokuwa katika jaribio la kutoroka. Wawili hao wamekuwa miongoni mwa wafungwa wanne waliokuwa wakisafirishwa hadi gereza la Siaya. Aidha wafungwa wawili waliosalia walitumia hali ya suitafahamu iliyokuwapo kutoroka. Afisa mkuu wa polisi katika eneo hilo Hussein Hassan amethibitisha kisa hicho. Msako dhidi ya wafungwa waliotoroka unaendelea, huku ikiaminika kuwa huenda wamejificha karibu na soko la Segere, kata ya Alego. Wafungwa wengine 19 waliosalia walisafirishwa hadi gereza hilo kutoka kituo cha polisi cha Ukwala chini ya ulinzi mkali.

    0 Responses

    Posted on April 16, 2013 na Mate Tongola