CORD kuwateua wajumbe wengine kwenye kamati ya pamoja na Jubilee

Muungano wa CORD siku ya Alhamisi utatoa upya orodha ya majina ya watakao uwakilisha kwenye kamati ya mazunguzo kuhusu hatima ya makamishna tisa wa Tume ya Uchaguzi, IEBC. Muungano huo hivyo basi umeondoa orodha ya majina ya walioteuliwa awali. Kinara wa CORD Raila Odinga amesema majina hayo yatatathminiwa upya kabla ya orodha nyingine kuwasilishwa.
Inaarifiwa hatua hii inafuatia tofauti miongoni mwa viongozi wa vyama vya Wiper na FORD Kenya huku baadhi wakilalamikia ukosefu wa usawa wa jinsia katika orodha hiyo.
Ford Kenya inasisitiza kwamba Seneta wa Kakamega, Bonny Khalwale anafaa kuchukua nafasi ya Mbunge wa Mogotio Hellen Sambili aliyekataa uteuzi huo. Hata hivyo wabunge wanawake wa Muungano huo wamepinga pendekezo hilo na kusema nafasi hiyo inafaa kuchukuliwa na mwanamke.
CORD iliwateua Mwakilishi wa Kike wa kaunti ya Mombasa Mishi Mboko, Seneta wa Siaya James Orengo, Seneta wa Makueni Mutula Kilonzo Jr, Mbunge wa Tongaren  Eseli Simiyu, Mbunge wa Suna Mashariki Junet Mohamed na Seneta wa Machakos Johnstone Muthama.
 
Na, Carren Omae

Related Topics

CORD IEBC